Friday, August 26, 2011

Adebayor atua Spurs kwa mkopo

Klabu ya soka ya Tottenham, imethibitisha kuwa imefanikiwa kumsajili mchezaji wa zamani wa mahasimu wao wakuu, Arsenal, Emanuel Adebayor, kwa mkopo toka klabu ya Manchester City.
Usajili wa Adebayor, umekuja katika kipindi ambacho alikuwa kwenye hatihati ya kutokuwa na timu maalum ya kuchezea baada ya kocha wa Manchester City, Roberto Mancini, kunukuliwa hivi karibuni akisema kuwa mshambuliaji huyo raia wa Togo, hakuwa tena na nafasi katika kikosi chake.
Adebayor mwenye umri wa miaka 27, alitua Manchester City kwa dau nono la paundi za kiingereza milioni 25 mwaka juzi lakini ghafla akakosa namba katika kikosi hicho na alitumia msimu uliopita akiitumikia Real Madrid ya Uhispania kwa mkopo, ambapo wakati wa kampeni ya miamba hao wa Hispania katika Ligi ya mabingwa wa Ulaya, Adebayor akiwa na kikosi cha Madrid, aliwatungua Spurs kwa mabao mawili na kuchangia kuwaondoa katika mashindano hayo.


No comments:

Post a Comment